Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi amesema kukamilika kwa jengo la Ofisi ya Uhamiaji Mkoa wa Mjini Magharibi kutaongeza ari na kasi ya utoaji wa huduma za Uhamiaji katika Mkoa huo na Manispaa zake zote tatu .

Rais Dk.Mwinyi amesema hayo alipoweka jiwe la Msingi jengo la Ofisi ya Uhamiaji Mkoa wa Mjini Magharibi tarehe 19 Aprili 2024 ikiwa ni shamrashamra za Miaka 60 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Aidha Rais Dk.Mwinyi amesema juhudi za Serikali zote mbili ni kubwa kuhakikisha Watanzania na Wageni wanaoitembelea nchini  wanapata huduma zilizo bora za Uhamiaji.

Halikadhalika Rais Dk.Mwinyi ameipongeza Idara ya Uhamiaji Tanzania kwa juhudi inazochukua kuhakikisha utoaji wa huduma bora na za kisasa kwa Wananchi, katika Mikoa na Wilaya zote nchini.

Vilevile Rais Dk.Mwinyi amesema gharama za mradi huo mpaka kukamilika ni shilingi bilioni 9.9 za kitanzania.

Kwa upande mwingine Rais Dk.Mwinyi ameeleza kuwa katika kipindi cha miaka 60 ya Muungano kupitia Idara ya Uhamiaji imepiga hatua kubwa  za mafanikio ikiwemo ya kuimarisha miundombinu ya utoaji huduma kwa kujenga Ofisi za kisasa Mikoa ya Unguja na Pemba na baadhi ya Wilaya zake.